Mashindano hayo ya kimataifa ya Qur'ani yanayofanyika kwa kaulimbiu ya "Kitabu Kimoja, Umma Mmoja" sambamba na kuanza sherehe za mwezi huu mtukufu wa Shaaban yanawajumuisha wasomaji (quraa) na waliohifadhi (hufadh) Qur'ani 258 kutoka nchi 84 na yataendelea hadi tarehe 25 mwezi huu wa Aprili.
Sherehe za ufunugzi, ambazo zimefanyika katika Ukumbi wa Sala wa Imam Khomeini MA, zimehutubiwa na Mkuu wa Shirika la Wakfu la Iran Hujjatul Islam Ali Mohammadi , Mshauri wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika Masuala ya Kimataifa, Dkt. Ali Akbar Velayati pamoja na Mkuu wa Shirika la Utangazaji la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, IRIB, Mhandisi Ali Askari.
Mashindano ya mwaka huu yatajumuisha Mashindano ya 35 ya Kimataifa ya Qur'ani Tukufu ya Iran (ya kawaida maalumu kwa ajili ya wanaume) na pia kutakuwa na mashindano mengine ya Qur'ani ya wanawake, ya wenye ulemavu wa macho, ya wanafunzi wa vyuo vikuu na ya wanachuo wa vyuo vya kidini.
Mashindano ya Kimataifa ya Qur'ani ya Iran, ambayo yatafanyika katika miji mitatu ya Tehran, Mashhad na Qum, ni tukio kubwa zaidi linalohusiana na Qur'ani katika Ulimwengu wa Kiislamu na yamekuwa yakiimarika kila mwaka.