IQNA

Iran yavunja njama ya magaidi wakufurishaji mjini Tehran na mikoa mitatu

11:24 - June 22, 2016
Habari ID: 3470409
Waziri wa Usalama Iran Mahmoud Alavi amesema magaidi wakufurishaji waliokamatwa hivi karibuni walipanga kutekeleza mashambulizi katika maeneo 50 kote Iran.

Akizungumza Jumanne, Alavi alisema katika oparesheni kadhaa za usalama mapema katika wiki za hivi karibuni, magaidi 10 Wakufurishaji walikamatwa Tehran na katika mikoa mingine mitatu ya kati mwa Iran.

Ameongeza kuwa, magaidi hao walipanga kuripua mabomu kwa njia ya 'remote control' na pia kutekeza hujuma za kujilipua na kwa mabomu ya kutegwa garini katika maeneo yenye msongamano mkubwa.

Amesema imebainika kuwa magaidi hao walikuwa tayari wameshaainisha maeneo 50 ya kutega mabomu na kwamba tayari walikuwa na kilo 100 za mada za milipuko huku vikosi vya usalama vikifanikiwa kuzuia tani mbili za mada za miripuko ambazo magaidi walipanga kuingiza nchini.

Siku ya Jumatatu Ali Shamkhani, Katibu wa Baraza Kuu la Usalama wa Taifa la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alisema vikosi vya usalama nchini vimetibua njama ya kutekelezwa shambulizi la kigaidi hapa mjini Tehran na kuwatia mbaroni watuhumiwa kadhaa wa njama hizo za kigaidi. 

Jumatatu iliyopita, Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu la Iran IRGC lilitekeleza operesheni maalumu na kuangamiza timu ya magaidi watano wa kundi la kigaidi la PJAK kaskazini magharibi mwa nchi. Taarifa ya IRGC ilisema magaidi hao waliuawa kufuatia operesheni maalumu ya kikosi cha nchi kavu cha jeshi hilo karibu na mji wa Sardasht, ambapo wanajeshi wa Iran walifanikiwa kunasa silaha kadhaa na nyaraka za siri.

Mwezi uliopita wa Mei, Mahmoud Alavi, Waziri wa Usalama wa Iran alisema vikosi vya usalama nchini vinafuatilia kikamilifu nyendo za maadui wanaopanga kufanya hujuma za kigaidi katika ardhi ya Jamhuri ya Kiislamu na kwamba maafisa usalama nchini hadi sasa wamefanikiwa kusambaratisha makundi 20 ya kigaidi.

/3508759

captcha