Ikiwa imesalia miezi 15 mpaka uchaguzi ufanyike hapo Desemba 2024 UNMISS wanasema lengo la kuandaa makongamano hayo ni kujenga utamaduni wa kuwa na mazungumzo thabiti, kutatua changamoto zinazowakabili kuhusu utawala bora na kujenga kuaminiana miongoni mwa wanasiasa na jamii wanazozitumikia.
Akiwa katika moja ya majukwaa huyo katika mji mkuu wa Juba Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini ambaye pia ni Mkuu wa UNMISS, Nicholas Haysom aliwaambia washiriki kuwa kuna udharura kwa wananchi na vyama vya siasa, kuelewa masuala ya uchaguzi.
Si wanasiasa pekee wanaohudhuria makongamano hayo bali pia wasomi ambao wamehimiza umuhimu wa kuwa na ushiriki mkubwa wa umma katika michakato ya amani, pamoja vyama vya siasa kuwa na ushindani imara.
Msomi maarufu wa Sudan Kusini Adwak Nyaba anasema: “Vyama vya siasa vinapaswa kuhimiza elimu ya kisiasa ili kuongeza ufahamu wa kijamii na ufahamu wa kisiasa wa wananchi. Ni kutokana na kuwepo kwa ufahamu wa kisiasa na watu wanaozingatia siasa kunakowezesha uwepo wa serikali za kidemokrasia. Ikiwa watu hawana ufahamu kabisa wa kisiasa, huwezi kuzungumzia utawala wa kidemokrasia, au huwezi kuzungumzia demokrasia.”
Wanasiasa wamehimizwa kufikia makubaliano ya masuala muhimu haswa kuhusu uanzishwaji wa taasisi muhimu ambazo ni Baraza la Vyama vya Siasa, Tume ya Kitaifa ya Marekebisho ya Katiba na Tume ya Kitaifa ya Uchaguzi.
Hivi karibuni Rais wa Sudan Kusini, Salvar Kiir alitaka nchi yake kuondolewa vikwazo vya silaha akieleza ili iwezi kusimamia uchaguzi kwa njia bora.
Akihutubia katika Mjadala Mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa uliofanyika mwezi Septemba, Rais huyo alisema “tunatoa wito kwa Umoja wa Mataifa kutuondolea vikwazo vya silaha vilivyowekwa kwa nchi yetu ili kusaidia utekelezaji wa amani na kulinda uchaguzi.”
Alibainisha kwamba “marufuku ya silaha iliyowekwa dhidi yetu imekwamisha utekelezaji wa mipango ya usalama kwasababu utekelezaji madhubuti wa vikosi vya pamoja hautaweza kutekelezwa bila silaha”.
3485357