Sura ya 12 ya Qur'ani Tukufu ni Sura Yusuf. Nabii Yusuf (AS) alikuwa nabii wa Bani Israel (Waisraeli). Alikuwa mwana wa Yaqub na aliota ndoto akiwa na umri wa miaka 9 kwamba nyota 11, jua na mwezi vinamsujudia. Ndoto hii inaonyesha hatima yake. Alipokuwa mtawala wa Misri, ndugu zake waliomtupa ndani ya kisima walimsujudia na kumtukuza baada ya miaka mingi.
Sura Yusuf ni sura ya Makki (iliyoteremka Makka). Imo katika Juzuu za 12 na 13 za Qur’ani Tukufu na ina aya 111. Ni Sura ya 53 iliyoteremshwa kwa Mtukufu Mtume (SAW).
Sura hii inasimulia kisa cha Nabii Yusuf (AS) kwa undani na kwa mujibu wa aya ya 3, ni Ahsan al-Qasas (simulizi nzuri zaidi). Hiyo ni kwa sababu inafikia lengo la simulizi za Qur'ani, yaani kujifunza darsa na ibra, katika ngazi ya juu kabisa
Kisa kinaanza na ndoto ya Yusuf (AS). Kisha inaeleza kwa kina kuhusu wivu wa ndugu zake na namna walivyomtupa kisimani. Sehemu nyingine za kisa hicho ni pamoja na kuokolewa Yusuf kisimani na namna alivyouzwa Misri, na akiwa hukoo namna Zuleikha alivyompenda, kisha kufungwa kwake, tafsiri yake ya ndoto ya mtawala wa Misri, kuwa mtawala wa Misri, na safari za ndugu zake na baba kwenda Misri.
Lengo la sura hii ni kutoa somo kwamba Mwenyezi Mungu atawapa hadhi na baraka za hali ya juu wale wanaobaki imara na kudumisha Ikhlasi (nia safi) yao mbele ya matatizo na masaibu.
Allamah Tabatabi, katika tafisri yake maarufu ya Qur’ani Tukufu ijulikanayo kama Tafsir al Mizan, anasema kuwa lengo kuu la Sura Yusuf ni kudhihirisha jinsi Mwenyezi Mungu anavyowapenda na kuwasaidia wale wenye imani na moyo safi na kwamba ikiwa mtu ana imani ya kweli, Mungu Mwenyezi atamsaidia na kumunezi katika hali ngumu zaidi.
Miongoni mwa mafunzo muhimu zaidi ya Sura hii ni wito wa kuwa na subira, ushupavu na uthabiti mbele ya matatizo na masaibu na kubakia katika hali ya utakasifu mbele ya matamanio ya dunia. Katika hali hiyo, Mwenyezi Mungu ameahidi kuwa atawalipa waja wema ambao wametenda amali njema.