Viongozi hao ambao walikusanyika katika mkutano katika kitongoji cha Detroit, walisema jinsi Biden alivyoshughulikia vita vya Israel na Palestina kunaweza kumgharimu kura za jumuiya ya Waamerika wa Kiarabu, jambo ambalo linaweza kuleta mabadiliko katika uchaguzi wa rais wa 2024.
Mkutano huo ulifanyika Dearborn, jiji lenye Waislamu wengi zaidi nchini Marekani.
Viongozi hao walitoka Michigan, Minnesota, Arizona, Wisconsin, Florida, Georgia, Nevada na Pennsylvania.
Mashambulio ya anga na ya ardhini ya utawala haramu wa Israel kwenye Ukanda wa Gaza uliozingirwa yamesababisha vifo vya zaidi ya Wapalestina 15,500 wengi wao wakiwa wanawake na watoto.
Marekani ni muungaji mkono mkuu wa utawala haramu wa Israel katika vita vyake dhidi ya Wapalestina na hivyo kusitasita kwa Biden kutaka kushinikiza Israel isitishe vita kumeharibu uhusiano wake na jumuiya ya Waislamu wa Marekani kiasi cha kutorekebishika tena, alisema Jaylani Hussein, mratibu wa mkutano huo wa Minneapolis.
"Familia na watoto wanaangamizwa na dola zetu za ushuru," Hussein alisema. "Tunachoshuhudia leo ni msiba juu ya msiba."
Hussein, aliliambia shirika la habari la Associated Press: "Hasira katika jamii yetu ni kubwa mno. Moja ya mambo ambayo yalitukera zaidi ni ukweli kwamba wengi wetu tulimpigia kura Rais Biden. Hata nilikuwa na tukio moja ambapo kiongozi wa kidini aliniuliza, 'Nitapataje kura yangu ya 2020 ili niiharibu?'
Michigan, Wisconsin na Pennsylvania yalikuwa majimbo muhimu ambayo Biden alishinda mnamo 2020, na kumsaidia kumshinda Rais wa zamani Donald Trump.
Takriban Wamarekani milioni 3.45 wanajitambulisha kuwa Waislamu, au 1.1% ya wakazi wa nchi hiyo, na wana mwelekeo wa kuegemea upande wa chama cha Democrats, kulingana na Kituo cha Utafiti cha Pew.
Lakini viongozi wa Waislami sasa wanasema kwamba uungwaji mkono wa jumuiya hiyo kwa Biden umetoweka kufuatia mauaji ya raia wa Palestina huko Gaza.
3486265